Monday, May 21, 2012

Watendaji Wa Kata Na Vijiji Walia Na Wanasiasa

Na Mwandishi Wetu
 Bukoba
VIONGOZI ngazi ya juu na wakisiasa wametakiwa kutoa ushirikiano kwa watendaji wa vijiji na kata ili kufanikisha shughuli nyingi za maendeleo ya jamii kukamilika kwa wakati.

Ushauri huo,umetolewa na watendaji wa vijiji na kata ndani ya halmashauri ya wilaya ya Bukoba,waliokuwa wakihudhuria semina ya kikazi ili kuwawezesha kutambua na kufuata wajibu wao katika shughuli zao za kila siku iliyofanyika katika vituo viwili vya Maruku na Lyamahoro.

Watendaji hao walibainisha kuwa shughuli zao hasa za kuhimiza na kukusanya michango zinakuwa ngumu na kuonekana kuleta kero kwa jamii kutokana na baadhi ya viongozi wa kisiasa kuitisha mikutano yao na kuanza kupokea kero za wananchi kwa madai wao ni watetezi,hivyo na kusababisha zoezi la kuimiza maendeleo kwenda kwa kusuasua.

"Tatizo kuu la jamii yetu kutohudhuria mikutano ya hadhara ni kutokana na wanasiasa wetu,kufika katrika mikutano yao na kuomba kusikiliza kero za wananchi,na mwisho kuwataka wananchi kutokubali lolote linalohusu masuala ya maendeleo hasa kuchangia"alisema Abdallah Rwabigimbo,afisa mtendaji kata Katoma.

Alisema kuwa mara nyingi jamii inawaona watumishi hawa kama ni sehemu ya kuwanyanyasa,jambo ambalo si kweli na linawafanya kuishi kwa mashaka juu ya maisha yao ya kila siku,na kusababisha jamii kuacha kuhudhuria mikutano pale wanapoitisha juu ya kupewa taarifa juu ya mapato na matumizi.

Hata hivyo,wameomba serikali kuangalia ni jinsi gani itaweza kuwapatia motisha viongozi wao wa kuchaguliwa yaani wenyeviti wa vitongoji ili kuwezesha kazi zao kufanyanyika vizuri na kwa ushirikiano mwema.

"Serikali iangalie jinsi gani inaweza kuwapatia motisha wenyeviti wa vitongoji ili kuharakisha shughuli za maendeleo,kwani wakati mwingine shughuli zetu zinakwama kutokana na viongozi hawa kutokuwa na mwamko kutokana na majukumu yao"alisema William Buberwa,afisa mtendaji kata Buhendangabo.

Kwa upande wake mratibu wa semina hiyo Philimon Magesa,ambaye pia ni afisa utumishi wa halmashauri ya wilaya Bukoba,aliwaasa watendaji hao kufuata sheria zilizopo hasa wakati wa kufanya shughuli zao za ulinzi na amani katika maeneo yao huku wakifatilia sana kanuni za maadili ya kazi.

Magesa alisema kuwa lengo kuu la semina hiyo,kuwapatia mafunzo watendaji hawa kufuata taratibu mbalimbali zilizo ndani ya kazi zao za kila siku na mada kuu ikiwa ni kufuata misingi ya utawala bora.

Semina hiyo iliyoendeshwa na mwezeshaji  Venance Shilingi,kutoka chuo kikuu cha Mzumbe iliwashirikisha jumla ya washiriki 120 wakiwa watendaji wa vijiji na kata ikiwa kata 29 na vijiji 94 vilivyo ndani ya halmashauri ya wilaya ya Bukoba.


MWISHO

No comments:

Post a Comment