Monday, May 28, 2012

Nape Akihutubia Wilayani missenyi

UVCCM wamtosa Nape Missenyi

na Audax Mutiganzi, Misenyi

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) wilayani hapa, kimekutana na wakati mgumu kwa kuumbuka mbele ya Katibu wa Taifa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye ambaye alikuwa mgeni rasmi wakati wa baraza la vijana la wilaya hiyo lililofanyika Ijumaa.
CCM imeumbuka baada ya vijana wake wilayani hapa kuonesha msimamo wao ndani ya chama hicho, kwa kususia baraza la vijana lililokuwa limeandaliwa, ambalo katika hali isiyo ya kawaida liliudhuriwa na wazee ambao ni pamoja na kina mama, kina baba na watoto.
Baraza hilo lililofanyika kwenye viwanja vya Mashujaa vilivyoko eneo la Bunazi yalipo makao makuu ya Wilaya Misenyi, vijana wengi wa CCM walisusia baraza hilo kwa madai ya kutokuwa na imani na serikali iliyoko chini ya CCM.
Wakati baraza la vijana likiendelea, vijana wengi, hasa ambao ni wakereketwa wa CCM, walionekana wakizurura ovyo, wakipita maeneo ambayo baraza lilikuwa likifanyika huku wengine wakiendelea na shughuli zao za kujipatia kipato.
Vijana waliozungumza na gazeti hili bila kutaja majina yao, waliokutwa maeneo ya Bunazi karibu kabisa na eneo lilikokuwa linafanyika baraza, walisema CCM haina mwelekeo, wamechoka nayo kwa kuwa kila siku inaendelea kuwatelekeza.
Kwa nyakati tofauti, walisema chama hicho kimeshindwa kabisa kulinda maslahi ya vijana badala yake kimekuwa kikiwatumia kila siku kufanikisha maslahi yake.
“Mimi ni mkereketwa wa CCM, mbunge wa sasa nimeshiriki kumpigia kampeni hadi akapita, wengi walioko ndani ya chama wapo kwa ajili ya kulinda maslahi yao wala si maslahi ya walio nyuma yao,” alisema mmoja wa vijana.
Kauli za vijana kususia baraza hilo, zilithibitika pale Katibu wa Umoja wa Vijana CCM wa Wilaya ya Misenyi, Philbert Ngemella aliposema mbele ya Nnauye kwamba vijana wamesusia baraza hilo kwa madai kwamba serikali iliyoko chini ya CCM haiwajali na imeshindwa kutafuta namna ya kuwawezesha kiuchumi.
Aidha, wakati wa baraza hilo, mzee Abdul Mwanandege alimtahadharisha Nape awe makini sana ili CCM isifie kwenye mikono yake.
Alisema CCM ni ya wanachama wote hivyo maamuzi ndani ya chama ni lazima yaende kulingana na matakwa ya wanachama.
Mwanandege alisema mpasuko ulioko ndani ya CCM kwa sasa unatokana na maamuzi yanayotolewa, ambayo hayaafikiwi na baadhi ya wanachama, na kuongeza kuwa, ili chama kiendelee kuwa imara kinahitaji umakini zaidi.
Naye Nape akihutubua baraza hilo la vijana alikiri mpasuko mkubwa ndani ya CCM, akisema ndani ya chama kuna mamluki, ambao ndio chanzo cha mpasuko.
“Watu hao tunao ndani ya chama na ndio wanatuvuruga ila tutaendelea kukabiliana nao hata kama chama kitabaki na mtu mmoja, tunataka watu safi wenye mapenzi ya dhati na chama,” alisema.
Nnauye alisema CCM inaendelea na mkakati wake wa kuwaadabisha wale inaowabaini kuchangia mpasuko, na kwamba haitamfumbia macho mtu yeyote atakayeisaliti.
Aliendelea kusema kuwa, CCM haimbembelezi mwanachama yoyote abaki ndani ya chama.
“Nasema anayetaka kuhama ahame, hata kama nitabaki peke yangu chama kitaendelea kuwepo, CCM si mali ya matajiri, ni mali ya maskini,” alisema Nape kwa kejeli.
Kauli hiyo ya Nape ilipokelewa kwa hisia tofauti na wanaCCM wachache walioudhuria baraza hilo, baadhi bila kutaja majina yao, wakisema kwamba Nape anakimaliza chama kwa kauli zake.


No comments:

Post a Comment