Monday, May 21, 2012

Miaka 16 Tangu Kuzama kwa Mv Bukoba

 Meli ya Mv Bukoba ikizama usiku wa kuamkia tarehe 21,May,1996
 Mnara wa kumbukumbu ya abiria waliopoteza maisha uliopo eneo la Igoma Jijijini Mwanza.
 Kwa Hisani ya Bukoba Pamoja Blogspot

LEO ikiwa ni kumbukumbu ya miaka kumi na sita tangu kuzama kwa meli ya Mv Bukoba,baadhi ya wananchi wa Mkoa wa Kagera wamehoji utekelezaji wa ahadi ya Rais Kikwete ya ununuzi wa meli mpya.
Meli ya Mv Bukoba ilizama May 21,1996 na kusababisha vifo vya zaidi ya watu mia tisa,ambapo wakati wa kampeini za uchaguzi Mkuu mwaka 2010 Rais Kikwete alihaidi ununuzi wa meli mpya kama mbadala wa meli iliyozama.
Wakihojiwa kwa nyakati tofauti juu ya kumbukumbu ya tukio hilo baadhi ya wananchi wamesema hawajaona juhudi zozote za utekelezaji wa ahadi hiyo na kuwa tangu wakati huo usafiri wa majini umezorota.
Mmoja wa wananchi hao Selestine Mwebesa mkazi wa kijiji cha Ruhunga wilaya ya Bukoba alisema mbali na kupoteza ndugu mmoja katika ajali hiyo,hakuna jitihada zozote zinazoonekana katika utekelezaji wa ahadi ya rais Kikwete.
Alisema utekelezaji wa ahadi hiyo haupashwi kuchelewa kwani kuzama kwa meli ya Mv Bukoba iliongeza pengo la usafiri kati ya wananchi wa Mkoa wa Kagera na Mkoa wa Mwanza.
Pia mwananchi mwingine Pontian Kaiza mkazi wa Kijiji cha Kibeta nje kidogo ya mji wa Bukoba alisema pamoja na ahadi ya meli mpya kuonekana imewekwa kando,pia alidai kuna malalamiko mengi ya wananchi ambao hawakupata kifuta machozi kama kilivyodaiwa kutolewa na serikali.
Alisema mmoja wa jamaa zake aliyemtaja kwa jina la Joseph Peter ambaye alimpoteza mke wake katika ajali hiyo ni miongoni mwa wananchi wengi ambao hawakupata kifuta machozi kilichotolewa huku wengine wakilalamikia kiwango kidogo walichopewa.
Mmoja wa wananchi waliopona katika ajali hiyo David Mtensa mkazi wa mjini Bukoba wakati wa kumbukumbu ya tukio hilo mwaka jana alinukuliwa akiilalamikia Serikali juu ya kiwango kidogo cha fedha zilizotolewa kwa waathirika wa ajali hiyo.
Alidai kiasi cha shilingi laki moja kilichotolewa kwa abiria aliyenusurika na laki tano waliopoteza ndugu hakikulingana na madhara waliyopata kwa kuzingatia kuwa baadhi yao walikuwa wafanyabiashara waliolazimika kuanza upya.
Miongoni mwa ahadi nyingi alizozitoa Rais Jakaya Kikwete wakati akitafuta muhura wa pili wa uongozi ni ununuzi wa meli mpya,ambapo mpaka sasa hakuna jitihada za wazi zinazoonekana juu ya utekelezaji wa ahadi hiyo.

No comments:

Post a Comment