Sunday, March 4, 2012

POLISI WADANGANYWA NA ALIYEMUOZESHA BINTI YAKE

Na Mwandishi wetu
Bukoba
 
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Buhanga kata ya Buganguzi wilayani Muleba Nestory Samson(Cuf) aliyedaiwa kumuozesha mwanafunzi wa kidato cha pili amelipotosha jeshi la polisi mkoani Kagera kwakudai kuwa binti yake hakuwa na uwezo darasani.
 
Kwa mujibu wa maelezo yaliyothibitishwa na kamanda wa polisi mkoa wa Kagera Henry Salewi mzazi huyo amedai binti yake alimweleza kuwa hawezi kuendelea na masomo na hivyo kuamua kuondoka nyumbani.
 
Alidai binti yake ambaye pia hakufanya mtihani wa kidato cha pili mwaka huu alimwambia hayuko tayari kuendelea na masomo na hivyo kumruhusu kwenda sehemu yoyote na kuacha masomo.
 
Mbali na mwenyekiti huyo kukana madai ya kumuozesha binti yake aliyekuwa anasoma kidato cha pili sekondari ya Bukidea alisema mtoto wake alikwenda kutafuta kazi za ndani jijini Mwanza.
 
Aidha kamanda Salewi amesema kuwa mwenyekiti huyo baada ya kuibuka kwa taarifa za kumuozesha mtoto wake alifika na mwanafunzi huyo juzi katika kituo cha polisi Muleba na kutoa maelezo ya kutokuwa tayari kuendelea na shule kwa madai ya masomo kuwa magumu.
Mwanafunzi huyo ambaye jina lake linahifadhiwa aliacha masomo mwezi May huku kukiwa na taarifa za familia pamoja na ndugu wa karibu kufanya njama za kumtorosha na hivyo kukatisha masomo yake.
 
Hata hivyo Kamanda Salewi hakusema hatua zitakazochukuliwa endapo binti huyo ataendelea na msimamo wake kutokana na maelezo aliyoyatoa kituo cha polisi akiwa na mzazi wake.
 
Mwisho

No comments:

Post a Comment