Thursday, August 23, 2012

Taasisi Za Kidini Zakanusha Uamsho


Na:  Idara ya Habari,MAELEZO
Taasisi mbalimbali za kidini hapa nchini zilizopata usajili rasmi kwa Mrajis Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar zimekanusha kuhusika na tamko lililotolewa na Amiri Mkuu wa Jumuiya ya Uamsho, Sheikh Mselem Ali la Waislamu wa Zanzibar wagomee kushiriki katika Sensa ya Watu na Makaazi Kitaifa inayotarajiwa kufanyika Jumapili ijayo.

Wakizungumza na Katibu wa Mufti wa Zanzibar, Sheikh Fadhil Soraga Wawakilishi wa Taasisi hizo wamelaani tabia ya Uamsho ya kujipa Mamlaka ya kuzisemea Taasisi hizo.

Aidha,wameitaka Jumuiya ya Uamsho kuthibitisha ni kikao gani kilichokaa na kuzungumza na Taasisi za Kidini na kuamua kwa pamoja kutowa tamko hilo la kupinga kushiriki kwa Waislamu katika Sensa.

Aidha, wameihakikishia Afisi ya Mufti na Serikali kuwa watashiriki katika Sensa ili kusaidia maendeleo ya Zanzibar na kutatua baadhi ya migogoro ya kijamii na sio kujiingiza katika siasa na kupingana na Serikali kama ambavyo imekuwa ikifanya Jumuiya ya Uamsho.

Taasisi zimewataka Waislamu kushirikiana na Serikali na kuachana upotoshaji unaofanywa na Uamsho.

Aidha, wameitaka Jumuiya ya Uamsho kuachana mara moja kutumia kivuli cha umoja wa Taasisi za kidini Zanzibar wanapoamua mambo yao kwani Jumuiya hizo nyingi hazikubaliani na Sera yao ya fujo na vurugu.

Mwisho.
Imetolewa na:
Idara ya Habari(MAELEZO) Zanzibar
23/08/2012

No comments:

Post a Comment