Thursday, August 9, 2012

Nane Nane Ilivyofungwa Bukoba


Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe. Kanali Mstaafu Fabian I. Massawe afunga rasmi maonesho ya NANE NANE 2012 Mkoani Kagera yaliyofanyika katika viwanja vya Kyakailabwa nje kidogo ya Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba yaliyoanza tarehe 1-8/08/2012.

Katika kufunga maonesho hayo yaliyofana sana na kushirikisha wakulima mbalimbali kutoka katika Halmashauri za Wilaya na Manispaa katika mkoa wa Kagera Mhe. Massawe aliyekuwa mgeni rasmi alitembelea mabanda mabalimbali ya wakulima na biashara na kujionea shughuli mbalimbali za wajasiliamali na kilimo.

Akiongea na wakulima na wananchi waliohudhuria katika siku ya kilele cha NANE NANE 2012 mkoani Kagera Mhe. Massawe alisistiza sana miradi ya kilimo kumilikiwa na wananchi wenyewe pamoja na Halmashauri za Wilaya, aidha kushiriki katika vikao vya kuibua miradi ya maendeleo katika maeneo yao.

Ufugaji wa nyuki, Mhe. Massawe alitoa wito kwa wakulima kuanza ufugaji wa nyuki ili kujipatia kipato kutokana na kuuza asali. “Asali ya mkoa wa Kagera ni asali bora duniani ambayo ina kiwango cha hali ya juu, pia kimeanzishwa kiwanda cha kusindika asali mkoani Pwani, fugeni nyuki ina soko kubwa duniani kote.” Aliwasistiza wakulima Mhe. Massawe.

Maagizo; Aidha Mhe. Massawe alitoa agizo kwa Halmashauri za Wilaya kuhakikisha maonyesho yajayo ya mwaka 2013 wanaletwa wakulima wengi ili waweze kujifunza kuliko kuwaleta wachache wakati wakulima wengi wangependa kujifunza teknolojia na kilimo cha kisasa chenye tija.

Pia Mhe. Massawe aliiagiza kamati ya maandalizi ya NANE NANE 2012 Mkoa wa Kagera kuanzisha maonyesho ya mifugo (wanyama) ili na sekta ya mifugo iweze kupata hamasa ya kutoa elimu kwa wafugaji kujifunza kufuga kisasa kuondokana na ufugaji wa kienyeji usiokuwa na tija.

Aidha katika kumaliza hotuba yake Mhe. Massawe aliwasistiza wananchi kujiandaa na kuwa tayari kuhesabiwa katika sensa itakayofanyika Agosti 26, 2012 na kuwaomba wale wote wanaopotosha na kuhamasisha wananchi kutohesabiwa kuacha mara moja kwani zoezi hilo la sensa ni la kusaidia serikali kupanga mipango ya maendeleo ya wananchi wake.

Maonesho ya NANE NANE 2012 Mkoani Kagera yaliandaliwa na kuratibiwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera na Halmashauri ya Wilaya ya Missenyi ilichukua kikombe kwa kuchukua nafasi ya kwanza kiujumla kwenye maonyesho hayo.

Pia Mwenykiti wa maonesho hayo Bw. Kagombora alibainisha kuwa pamoja na maonesho hayo kufana lakini bado kuna changamoto zinazoukabili uwanja wa Kyakailabwa ambazo ni miundombinu ya Maji na Umeme ambazo bado zinatafutiwa ufumbuzi.




Mkuu wa mkoa wa Kagera Kanali Mstaafu, Fabian Massawe akiwa ameshikana mkono na katibu tawala wa mkoa wa Kagera wakikagua mabanda ya nanenane.




Baadhi ya wananchi wakijivinjali kwenye uwanja wa maonyesho ya nanenane.




Fisi alikutwa kwenye viwanja vya maonyesho ya nanenane Kyabailabwa.

No comments:

Post a Comment