Thursday, May 23, 2013

JK awahimiza Watanzania kulinda amani ya nchi

 Rais Jakaya Kikwete amewataka Watanzania kulinda na kudumisha amani ya nchi kwa kujiepusha na vikundi vya watu wanaochochea vurugu.

Hayo aliyasema jana alipokuwa akizungumza na wakazi wa Kata ya Migoli, Tarafa ya Isimani wakati wa kuweka jiwe la msingi kwenye Barabara ya Iringa - Dodoma ambapo alisema matukio ya hivi karibuni yanahatarisha amani ya nchi.
“Ndugu zangu kabla sijafikia tamati ningependa nizungumzie hili, nawaomba mdumishe amani na upendo. Taifa hili limedumu katika amani kwa muda mrefu, matukio ya hivi karibuni hayafurahishi…Wapo watu wanalala usiku na mchana wanapanga njama za kuvuruga amani ya nchi yetu, watu hawa wasipewe nafasi, wasisikilizwe kwani hawana nia njema na taifa letu,” alisema Kikwete.
Kikwete alisema Watanzania wakikataa kuwasikiliza, kuwafuata na kutenda wanavyotaka Tanzania itabaki kuwa nchi ya amani na mipango yao haitafanikiwa.
Kauli ya Kikwete imekuja huku kukiwa na matukio ya vurugu za kidini na matukio ya maandamano ya uharibifu wa mali yanayofanywa na baadhi ya makundi ya kidini nchini.
Akizungumzia uzinduzi wa ujenzi wa barabara hiyo ambao ni sehemu ya Barabara Kuu ya Kaskazini inayounganisha Iringa-Dodoma kwa kiwango cha lami, Kikwete alisema barabara ni ufunguo wa uchumi katika taifa lolote duniani.
“Wapo watu wanaohoji ni kwa nini tunatumia fedha nyingi kuwekeza kwenye ujenzi wa barabara, tungeweza kutumia fedha nyingi kwenye maeneo mengine, lakini pamoja na kwamba tumechelewa kuwekeza kwenye barabara bado kama nchi tuna nafasi ya kuunganisha nchi kwa barabara na kasi ya uchumi itakua,” alisema Kikwete.
Kikwete alifafanua kuwa kwa sasa Serikali yake imeweka kipaumbele katika ujenzi wa barabara na kuongeza kuwa ndiyo sababu barabara nyingi zinazounganisha miji mikubwa na zile za kawaida zimejengwa na nyingine zinaendelea kujengwa kwa kasi.
Alisema kutokana na hatua hiyo Serikali yake imeimarisha mfuko wa barabara ambapo wakati anaingia madarakani ulikuwa na kiasi cha Sh55 bilioni, lakini kwa kipindi cha miaka saba imefikia Sh430 bilioni na sasa mfuko huo unatarajiwa kutengewa Sh504 bilioni katika bajeti ya mwaka 2013/14.
Kikwete aliwataka wakazi wa Iringa na maeneo yote zinakojengwa barabara kushiriki, kuzitunza kwa kulinda miundombinu yake na kushukuru nchi wahisani kwa ujenzi wa miundombinu nchini.
Kuhusu umuhimu wa matumizi ya barabara alisema zitasaidia wakazi wa maeneo jirani kukuza uchumi na kuwataka kutumia fursa hiyo kufanya kazi za uzalishaji kwa bidiii ili waweze kunufaika na matunda ya barabara hizo.
Kwa upande wake Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli alisema Serikali itahakikisha makandarasi wote wanaoendelea na ujenzi wa barabara nchini wanakamilisha kazi zao kwa wakati na wanajenga kwa kiwango kinachotakiwa.

No comments:

Post a Comment